Monday, June 11, 2018

WATANZANIA TUSIKUBALI KUCHONGANISHWA-MAJALIWA




WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wasikubali kuchonganishwa na kwamba Serikali haiongozwi kwa misingi ya kidini bali imeziachia taasisi za kidini zifanye kazi kwa kuzingatia Katiba , Sheria za nchi na malengo yaliyokusudiwa katika uanzishwaji wake.

Aliyasema hayo jana jioni (Jumamosi, Juni 9, 2018) alipozungumza na viongozi na wananchi wa Mkoa wa Mwanza baada ya kushirikiana nao katika futari aliyowaandalia. Shughuli hiyo ilihudhuriwa na waumini wa dini mbalimbali.

Waziri Mkuu alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wake wanaishi kwa amani na utulivu, jambo litakalowawezesha kufanya shughuli zao kikamilifu, hivyo wasikubali kuchonganishwa kwa misingi yoyote.

“Nawaasa viongozi wa dini msikubali kutumia makundi mengine nje ya taasisi zenu kwa ajili ya kuwazungumzia masuala yenu kwa sababu watawachonganisha na Serikali ambayo haipo kwa ajili ya kugombana na taasisi yoyote,” alisisitiza.

Waziri Mkuu alisema jukumu kubwa la taasisi za kidini ni kuhakikisha wanawalinda waumini wao pamoja na kuwaongoza kwa kuwapa mafundisho mema yanayompendeza Mwenyezi Mungu, ambayo yatawawezesha kuishi kwa amani .

Alisema misingi ya amani na utulivu ikiwa pamoja na mshikamano walionao wananchi umesababisha Tanzania kupata heshima kubwa dunia kote, hivyo ni vema kila mwananchi ahakikishe suala la kudumisha amani linapewa kipaumbele.

Pia Waziri Mkuu  alisema amefurahi sana kujumuika na wananchi wa Mkoa wa Mwanza katika futari hiyo, ambapo aliwapongeza kwa kukamilisha uundaji wa kamani za amani kuanzia ngazi ya kata hadi mkoa.
Awali, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Bw. John Mongella amlishukuru Waziri Mkuu kwa ukarimu wake kwa kuwaalika wakazi wa Mwanza katika hafla hiyo, ambapo alisema Mwanza ni kitovu cha amani kwa kanda ya Ziwa na nchi za Maziwa Makuu. T

“Mwanza tumejipanga na tunashirikiana na taasisi zote kwenye njanja zote , tupo pamoja na tunashirikiana katika kuimarisha amani na utulivu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli kwa kutuamini na tunamuahidi tutafuata falsafa zake katika utendaji wetu,”.

Kwa upande wake, Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Amani ya Mkoa wa Mwanza na Askofu wa Kanisa la Charismatic Episcopal Church of Tanzania (CECT), Charles Sekelwa alisema wao wanaiunga mkono Serikali katika kudumisha amani na wataendelea kushirikiana nayo.

Alisema awali kulikuwa na changamoto ya matabaka ya kidini iliyobabisha na kutoelewana baina ya waislamu na wakiristo, ambapo kamati yao ilifanya kazi ya kuyasulisha na sasa hali ni shwari. “Matabaka ya kiimani yameisha na watu wa dini zote wanashirikiana vizuri,”.

Askofu Sekelwa alisema wao kama viongozi wa pande hizo mbili hawawezi  kukubali kuona kunakuwa na matabaka ya kiimani miongoni mwa waumini, hivyo watakikisha wanaendelea kuwafundisha waumini wao umuhimu wa amani.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Naibu Spika Dkt. Tulia Akson, Naibu Waziri waNchi, OR – TAMISEMI, Joseph Kakunda, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali baadhi ya wananchi wa mkoa wa Mwanza

Tuesday, July 19, 2016

MAJALIWA: MALIASILI NA UTALII JIPANGENI VIZURI



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii
kujipanga vizuri na kufanya mapitio ya idara zake hususan ya misitu baada ya kubainika kuwepo kwa matatizo makubwa.
“Eneo la misitu limekuwa na matatizo makubwa, watendaji wengi si waaminifu na sura ya wizara si nzuri miti mingi inakatwa na fedha haiingii Serikalini. Huu ni mgogoro mpya,” alisema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo jana alipokutana na watumishi wa wizara hiyo jana (Jumatatu, Julai 18, 2018) jijini Dar es Salaam, na kusisitiza kwamba hakuna sababu ya Serikali kuendelea kuwa na watumishi wasiokuwa na uaminifu, uadilifu na uwajibikaji.
Alisema lengo la mkutano huo ni kukutana na watumishi
kusikiliza changamoto zao, kukumbushana wajibu, pamoja na kutoa maagizo ili
yatekelezwe kwa utaratibu unaokubalika kisheria.

Alisema mtumishi ambaye atabainika kuwa haitendei haki nafasi yake kwa
kutokutimiza majukumu ipasavyo hana sababu ya kuwepo kwa sababu serikali
inapoteza fedha nyingi kuwalipa watu wasio na tija.

Waziri Mkuu alisema sababu inayoikosesha Serikali mapato ni
uwepo wa watumishi wasio waadilifu kwenye ofisi za Serikali ikiwemo Wizara
ya Maliasili na Utalii hivyo kuna umuhimu wa kuzisafisha.

Alisema kuna uvunaji mkubwa wa misitu kuliko upandaji huku asilimia 50 ya mapato yatokanayo na uvunaji huo yanapotea na kuisababishia Serikali hasara ambapo alihoji sababu ya wizara kushindwa kusimamia jambo hilo.

Katika hatua nyingine; Waziri Mkuu aliitaka wizara hiyo kupunguza idadi ya vizuizi vya ukaguzi wa mazao ya
misitu kwenye barababara mbalimbali baada ya kukosa tija kutokana na upotevu wa misitu unaotokea kila siku.

Alitoa mfano wa barabara ya kwenda mikoa ya kusini  kuanzia Dar es Salaam
ambapo alisema ina vizuizi visivyopungua sita na kila kizuizi kinatumika kwa ajili ya kukagua mazao ya misitu na maliasili inayotoka kuvunwa.

“Vizuizi vya katikati ya safari havina umuhimu na badala yake kuwe
na vizuizi mwanzo na mwisho ili rasilimali zingine zitumike kuongeza nguvu
na umakini wa ukaguzi kwenye vituo vichache vitakavyosalia,”.

“Kwa mfano ukitokea Ikwiriri kuja Dar, kuna vituo vya ukaguzi wa maliasili
visivyopungua sita, kuna Ikwiriri, Kibiti,  Jaribu Mpakani,Mkuranga, Vikindu  kote huku
wanakagua lakini linapofika kituo cha mwisho cha Mbagala linakutwa na makosa kwenye mzigo kwanini’’?

“Yule mkaguzi wa kwanza alifanya kazi gani? Kuna tatizo la uadilifu na
ninyi ni mashahidi, sasa naagiza ongezeni nguvu kwenye vituo vikuu vya
ukaguzi yaani mwanzo na mwisho,” alisema.

Aidha alisema ni muhimu kukawa na mabadiliko kwenye mfumo wa mauzo ya
misitu kutoka wa sasa (kuuza kwa eneo) na kuhamia kwenye mfumo wa mnada
ambao utaongeza mapato ya Taifa na utaweka uwazi.

Pia aliwataka watumie mashine za malipo za kielektroniki (EFD),wanapofanya mauzo ya mazao ya misitu ili
kuepusha matumizi ya daftari na risiti bandia ambazo hazitambuliwi na
wizara.

MAJALIWA: BARA LA AFRIKA BADO LINAKABILIWA NA CHANGAMOTO YA UPATIKANAJI WA MAJI


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Bara la Afrika bado linakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama hasa vijijini kwa sababu nchi zake bado hazijamudu kuunganisha huduma hiyo katika maeneo hayo.
Kufuatia hali hiyo, Waziri Mkuu amewataka wataalamu wa masuala ya maji watafute njia sahihi itakayowezesha kutatua tatizo hilo kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya maji vilivyoko.
Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo jana (Jumatatu, Julai 18, 2016) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere  jijini Dar es salaam wakati akifungua mkutano wa 10 wa Baraza la Mawaziri wa Maji wa Afrika (AMCOW) ambao unaokwenda sambamba na maadhimisho ya Wiki ya Maji Afrika.
“Tunategemea baada ya kumazika kwa mkutano huu wataalamu wetu wataondoka na maazimio mazuri ya kumaliza tatizo la maji katika Bara letu kwa kutumia mito na maziwa ili kufikisha maji kwa wananchi,” alisema.
Akizungumzia kwa upande wa Tanzania alisema,  suala la maji limepewa kipaumbele hata katika bajeti ya mwaka huu na kwamba Serikali itahakikisha maji yanapatikana katika maeneo yote ili kutimiza sera yake ya kila mwananchi kupata maji umbali usiozidi mita 400.
Kwa upande wake Rais Mstaafu wa Kenya Mwai Kibaki ambaye ni Mjumbe Maalumu wa UNESCO kwa ajili ya masuala ya maji Barani Afrika alisema maji ni muhimu kwa maendeleo ya uchumi, hivyo wataalamu wanatakiwa kuhakikisha huduma hiyo inapatika katika maeneo yote.
Mkutano huo  wa siku tano unahudhuriwa Mawaziri wa Maji kutoka nchi 45 za Afrika na unaongozwa na Waziri wa Maji na Mazingira wa Senegal Amadou Mansour Faye ambaye ni Rais wa AMCOW.
(mwisho)