Sunday, May 03, 2015

NMB YAKABIDHI HUNDI YA SH. BILIONI 1.5 KUCHANGIA MADAWATI


WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amepokea hundi ya mfano (dummy cheque) yenye thamani ya sh. bilioni 1.5 kutoka benki ya NMB zikiwa ni mchango wa taasisi hiyo kwenye kampeni ya uchangiaji madawati kitaifa.

Akizungumza na Waziri Mkuu ofisini kwake Magogoni jijini Dar es Salaam jana jioni (Jumatano, Aprili 29, 2015), kabla ya kukabidhi hundi hiyo, Kaimu Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB, Bw. Tom Borghols alisema wameamua kutoa mchango ili kusaidia kupunguza tatizo la uhaba wa madawati linalozikabili shule za msingi na za sekondari hapa nchini.

“Tunaelewa kwamba shule nyingi hapa nchini zinakabiliwa na uhaba wa madawati … tunaamini kuwa elimu bora inachangiwa pia na mazingira mazuri ya kusomea ikiwa ni pamoja na kukaa kwenye madawati wanapoandika. Kama sehemu ya mchango wetu kwa jamii (CSR), tumeamua kutenga sh. bilioni 1.5 ili zisaidie kupungua tatizo hilo,” alisema.

Akipokea mchango huo, Waziri Mkuu aliushukuru uongozi wa benki hiyo ulioambatana na Bw. Borghols kwa kuamua kusaidia juhudi za Serikali kutatua tatizo hilo. Alisema mchango huo ni mkubwa na anaamini kwamba utawachochea wadau wengine kuchangia juhudi za Serikali kutatua tatizo la madawati nchini.

“Nimecheki na watu wangu kwa kweli mahitaji ni makubwa lakini naamini mchango wenu utasaidia kupunguza tatizo la madawati kwa kiasi fulani. Tunawashukuru kwa uamuzi wenu wa kuchangia suala hili la kitaifa,” alisema.

Hadi sasa Serikali inahitaji kununua madawati 1,016,476 kwa ajili ya shule za msingi na za sekondari. Kati ya hayo, madawati 892,772 yanahitajika kwa ajili ya shule za msingi na madawati 123,704 yanahitajika kwa ajili ya shule za sekondari.

Madawati hayo yote yataigharimu Serikali kiasi cha sh. bilioni 91.4/- kwa gharama ya sh. 90,000/- kwa kila dawati.

Hata hivyo, Serikali iliamua kutenga fedha za chenji ya RADA ili zitumike kununua madawati na vitabu. Fedha hizo, zilisaidia kununua madawati 168,163 kwa bei ya sh. 90,000/- kwa dawati moja.

(mwisho)

IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU,

No comments:

Post a Comment