Monday, October 05, 2015

SINA KINYONGO NA DK. MAGUFULI - PINDA *Ataka watu watunze shahada zao


MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambaye pia ni mjumbe
wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), Mhe. Mizengo Pinda amesema yeye hana
kinyongo na uteuzi wa Dk. John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais kwa
tiketi ya CCM kwa sababu anaamini kuwa Mungu alikwishamuandaa.

“Tulikuwa wengi kwenyhe kinyang’anyiro cha urais lakini Makamu wa Rais
ametolewa, Waziri Mkuu aliyepo ametolewa, Mawaziri Wakuu wastaafu
wametolewa, Majaji na mabalozi wametolewa, mawaziri wengine
wametolewa; hivi ni kwa nini useme kwamba wewe tu ndiye unayefaa
kuteuliwa? Ni kwamba Mungu alikwishamuandaa mmoja wetu,” alisema.

Ametoa kauli hiyo jana (Jumamosi, Oktoba 3, 2015) wakati akizungumza
kwa nyakati tofauti na wakazi wa jimbo la Mpanda Vijijini kwenye
mikutano minne ya hadhara iliyofanyika katika kata za Kasekese,
Kapalamsenga, Karema na Ikola.

“Magufuli ni muadilifu, ni mchapakazi, hana blah blah za kisiasa na
hapendi rushwa. Ni mtu anayetaka kuona matokeo na mwenye kujali watu
wanyonge. Nimefanya naye kazi kwa muda mrefu, ninamfahamu, ninaomba
mumpe kura ya ndiyo ifikapo terehe 25 Oktoba,” alisema Mhe. Pinda
wakati akimuombea kura Dk. Magufuli.

Akizungumzia mafanikio ya serikali ya awamu ya nne, Mhe. Pinda alisema
Serikali ya CCM imefanya kazi nzuri kwa kufungua barabara za vijijini
akitoa mfano wa barabara ya Mpanda hadi Karema ambayo alisema
imeboreshwa tofauti na ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.

“Wakati huo ukitoka Mpanda kuja Karema ilimchukua mtu hadi siku tatu
wakati ni umbali wa km. 150 tu… leo hii mtu anatoka Karema hadi Mpanda
na kuunganisha mabasi ya Mwanza siku hiyo hiyo,” alisema.

Alisema katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015, Serikali ya awamu ya
tano imepanga kujenga reli mpya ya viwango vya kimataifa (standard
gauge) kutoka Kaliua kupitia Mpanda hadi Karema. Alisema anaamini reli
hiyo itakuwa ni kiungo cha kuleta maendeleo ya haraka kwenye ukanda
huo wa Magharibi.

Alisema Seikali itaendelea kuwaletea maendeleo wanandhi ikiwemo
kubotesha huduma za maji, umeme na mawasiliano ya simu.

Aliwataka wakazi wa jimbo hilo watunze shahada za kupigia kura na
wasikubali kurubuniwa na mtu yeyote iwe kwa fedha au kitu chochote.
“Usikubali kumpa mtu shahada yaka hata kama ni motto wako. Ninawasihi
mjitokeze kwa wingi siku ya kupiga kura wala msisikilize vitisho vya
mtu yeyote kwamba hakutakuwa na amani,” alisema.

Mhe. Pinda alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la
Mpanda Vijijini, Bw. Selemani Moshy Kakoso pamoja na madiwani wa kata
zote nne.

Akiwa Karema, Mhe. Pinda alipokea kadi za wanachama waliorejea CCM
kutoka vyama vya CHADEMA NA ACT Wazalendo.

No comments:

Post a Comment